Wafanyakazi wa umma Nigeria waanza mgomo wa nchi nzima
Wanachama wa miungano mikuu ya wafanyakazi wa umma nchini Nigeria wameanza mgomo wa taifa zima leo Alkhamisi, baada ya mazungumzo kati yao na serikali kuhusu nyongeza ya kima cha chini cha mshahara kugonga mwamba.
Aghalabu ya ofisi za serikali na benki zimesalia kufungwa hii leo hususan katika mji mkuu Abuja.
Mji huo pamoja na viunga vyake haujawa na shughuli nyingi za kila siku hii leo.
Joe Ajavero, Mkuu wa Kongresi ya Umoja wa Wafanyakazi Nigeria amebainisha kwamba, wanachama wa muungano huo wanafanya mgomo huo kulalamikia mazingira mabaya ya kazi na mishahara midogo wanayopewa wafanyakazi; akisisitiza kuwa, kuna uwezekano mgomo huo ukaathiri kwa kiasi kikubwa sekta tofauti zikiwemo za mafuta na usafiri wa anga.
Nigeria licha ya kuwa moja ya nchi tajiri zaidi barani Afrika na yenye utajiri wa mfuta, lakini mbali na changamoto za usalama inakabiliwa pia na mtikisiko mkubwa wa kiuchumi.
Mwezi Julai mwaka huu, maelfu ya maofisa wa polisi kaskazini mashariki mwa Nigeria, eneo linalokabiliwa na machafuko ya kundi la Boko Haram, waliandamana wakilalamikia kucheleweshewa mishahara yao.