Wahajiri 300 waokolewa katika maji ya pwani ya Libya
Shirika moja lisilo la kiserikali nchini Uhispania limeripoti kuwa wahajiri haramu 300 wameokolewa katika maji ya pwani ya Libya.
Shirika la Proactive Open Arms la nchini Uhispania limeongeza kuwa wanawake na watoto ni miongoni mwa watu waliookolewa katika operesheni hiyo ya uokozi.
Kwa mujibu wa Shirika la Kimataifa la Uhajiri, njia ya majini ya kutoka Libya kuelekea nchi za Ulaya ikiwemo Italia na Malta, ndiyo njia hatari zaidi kwa maafa ya roho za watu inayotumiwa na wahajiri waharamu kutoka nchi hasa za Kiafrika kwa safari za kuelekea barani Ulaya kwa lengo la kutafuta maisha mazuri.
Hata hivyo ripoti zinaeleza kuwa asilimia kubwa ya wahajiri hao huwa hawafiki wanakoelekea, bali huishia mikononi mwa magenge ya magendo ya binadamu, kuzama baharini au kupigwa mnada masokoni na kuuzwa kama watumwa.
Kwa mujibu wa Shirika la Kimataifa la Uhajiri, tangu ulipoanza mwaka huu wa 2018 hadi sasa, wahajiri zaidi ya 1,300 wamefariki dunia katika safari hizo.
Hii ni pamoja na kwamba serikali za nchi za Ulaya ikiwemo Italia zimekuwa zikichukua hatua kali dhidi ya uingiaji wa wahajiri katika nchi zao.../