Walioaga dunia baada ya jengo kuporomoka Nigeria wafika 20
Kamishna wa Afya katika jimbo la Lagos nchini Nigeria amesema idadi ya watu waliopoteza maisha baada jengo kuporomoka imeongezeka na kufikia watu 20.
Jide Idris ameyasema hayo leo Ijumaa na kuongeza kuwa, watu 45 wamenusurika katika mkasa huo. Kwa mujibu wa afisa huyo wa afya wa Nigeria, wanafunzi 10 na watu wazima wanne ni miongoni mwa majeruhi na hivi sasa wanaendelea kupatiwa matibabu katika hospitali za mji wa Lagos.
Jengo hilo la ghorofa tatu lililokuwa na shule ya msingi, maduka, na nyumba za kuishi lilianguka Jumatano iliyopita.
Daktari mmoja ambaye hakutaka kutaja jina lake amesema, kati ya watu waliofariki dunia kwenye ajali hiyo, ni mwanamke mjamzito.
Shule ya msingi iliyokuwepo katika jengo hilo ilikuwa na wanafunzi 172 walioandikishwa.
Ingawaje sababu ya kuanguka kwa jengo hilo haijabanika kufikia sasa, lakini kwa mujibu wa vyanzo vya habari nchini Nigeria, jengo hilo la ghorofa tatu lililoanguka ni kongwe na lina takriban miaka 30 tangu lijengwa.