9 wauawa katika shambulio la silaha Nigeria
Vyombo rasmi nchini Nigeria vimetangaza kuwa watu 9 wameuawa katika shambulio jipya la watu waliokuwa na silaha katika kijiji kimoja kaskazini mwa nchi hiyo.
Gavana wa Jimbo la Kaduna kaskazini mwa Nigeria ambalo daima linashuhudia machafuko na mapigano ya kikabila amesema katika taarifa kwamba watu hao tisa waliuawa jana alfajiri na watenda jinai katika kijiji cha Namdo kilichoko katika wilaya ya Sangha. Taarifa hiyo ambayo imelaani vikali mauaji hayo imesema kwamba washambuliaji pia waliteketeza nyamba kadhaa katika kijiji hicho. Jimbo la Kaduni linaunganisha eneo la kaskazini ambalo wakazi wake wengi ni Waislamu na la kusini ambalo wakazi wake wengi ni Wakristo.
Jimbo hilo limekuwa uwanja wa ghasia za mara kwa mara kati ya wafugaji ambao wengi ni Waislamu na wakulima ambao wengi ni Wakristo. Machafuko hayo ambayo kimsingi hutokana na ugomvi juu ya malisho na maji, katika siku za hivi karibuni yamechukua sura ya mapigano ya kikabila na kidini. Rais Muhammad Buhari wa nchi hiyo katika taarifa aliyoitoa jana Jumamosi alilaani machafuko hayo na kusisitiza kwamba matatizo yanayoikabili nchi hiyo hayawezi kutatuliwa kupitia machafuko ya aina hiyo.