Ethiopia yarusha satalaiti yake ya kwanza katika anga za mbali
Ethiopia leo Ijumaa imerusha satalaiti yake ya kwanza katika anga za mbali na kujiunga na nchi kadhaa za Kiafrika ambazo zina miradi ya anga za mbali kwa malengo ya ustawi na sayansi.
Maafisa wa ngazi za juu wa serikali ya Ethiopia walikusanyika katika kituo cha Anga za Mbali cha Entoto karibu na mji mkuu Addis Ababa ili kutizama mubashara satalaiti hiyo inayojulikana kwa jina la ETRSS-1, ikirushwa katika anga za mbali kutoka katika kituo kimoja cha kurusha satalaiti nchini China.
Naibu Waziri Mkuu wa Ethiopia, Demeke Mekonnen amezungumza baada ya kushuhudia satalaiti hiyo ikirushwa katika anga za mbali na kusema: "Huu ni msingi wa safari yetu ya kihistoria ya kuelekea katika ustawi."
Solomon Belay, Mkurugenzi wa Taasisi ya Sayansi ya Anga za Mbali Ethiopia amesema satalaiti hiyo imeundwa kwa ushirikiano wa wahandisi wa China na Ethiopia huku serikali ya China ikichangia dola milioni 6 kati ya milioni saba zilizohitajika kuunda satalaiti hiyo.
Amesema, kutumwa satalaiti hiyo katika anga za mbali kutakuwa na mchango mkubwa katika ustawi wa usalama wa chakula, ubunifu wa ajira, ustawi wa teknolojia, mamlaka ya kujitawala, kupunguza umasikini na kila kitu ambacho Ethiopia inahitajia kufikia maendeleo endelevu.