Watu zaidi ya 20 wapoteza maisha katika ajali ya boti DRC
Watu wasiopungua 20 wamepoteza maisha kufuatia ajali ya boti huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo katika Mto Kasai.
Kwa mujibu wa taarifa Idara ya Usafiri wa Majini katika kijiji cha Tshimbinda, ajali hiyo ilijiri baada ya moto kutokea baada ya mmoja wa wahudumu kuwasha sigara wakati mafuta yalipokuwa yakiwekwa katika injini.
Waokoaji wanaendelea na kazi ya uokozi kuwatafuta watu waliotoweka katika eneo hilo la kati mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Boti hiyo ilipata ajali Disemba 24 karibu na kijiji cha Tshimbinda yapata kilomita 3 kutoka mji wa Tshikapa katika mkoa wa Kasai. Taarifa zinasema miongoni mwa walipoteza maisha ni mmiliki wa boti hiyo aliyetambuliwa kwa jina la Shakis.
Ajali hutokea mara kwa mara kwenye mito nchini humo, ambapo nyingi zimerikodiwa tangu mwanzoni mwa mwaka. Sababu kuu ya ajali za boti nchini humo kwa kawaida ni hali mbaya boti, kujazwa abiria kupita kiasi na kuzeeka kwa boti hizo.