Corona imeua watu karibu 800 hadi sasa barani Afrika
Kituo cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa cha Umoja wa Afrika kimesema takriban watu 800 wamepoteza maisha kutokana na ugonjwa wa Covid-19 unaosababishwa na virusi vya Corona barani Afrika.
Kwa mujibu wa taasisi hiyo ya kikanda, watu 793 wameaga dunia kutokana na Corona katika nchi 52 za Afrika kufikia sasa.
Kwa mujibu wa takwimu mpya za kituo hicho, zaidi ya watu 15,000 wameambukizwa virusi hivyo hadi sasa barani humo huku kukiweko na ishara za kuongezeka maambukizo hayo.
Shirika la Afya Duniani (WHO) limesema Algeria inaongoza kwa idadi ya vifo na maambukizo barani Afrika na kwamba hadi sasa, watu 313 wamekufa kwa Corona katika nchi hiyo ya kaskazini mwa Afrika na walioambukizwa ni 1,983.
Misri ambayo ni nchi nyingine ya Kiarabu ya kaskazini mwa Afrika inashika nafasi ya pili kwa vifo ambapo watu 159 wameaga dunia kufikia sasa, huku Morocco ikirekodi vifo 126 vya Corona hadi sasa.
Umoja wa Afrika umetahadharisha juu ya kuenea zaidi virusi vya Corona barani Afrika, huku ukitoa mwito wa kuchukuliwa hatua za haraka za kukabiliana na ueneaji wa virusi hivyo.