Mama na wanawe wawili wafa njaa nchini Somalia
Mwanamke mmoja na watoto wake wawili wameaga dunia kutokana na makali ya njaa na kiu huko kusini magharibi mwa Somalia.
Mkuu wa Wilaya ya Rabdhure katika Mkoa wa Bakool, Mohamed Kheyr Salaad aliwaambia waandishi wa habari jana Jumapili kuwa, wilaya hiyo imeathiriwa vibaya na janga la ukame, na yumkini watu wengine wengi wameaga dunia kutoka na baa la njaa.
Salaad ameeleza kuwa, hatua ya wanachama wa kundi la kigaidi la al-Shabaab kuliwekea mzingiro eneo hilo katika kipindi cha miaka minane iliyopita, imewaongezea mashaka wakazi wa eneo hilo, kwa kuwa misaada ya kibinadamu haiwezi kupelekwa kupitia barabara.

Kwa mujibu wa Mpango wa Chakula wa Umoja wa Mataifa (WFP), watu milioni 13 katika eneo la Pembe ya Afrika ikiwemo Somalia wanakabiliwa na njaa kali.
Aidha Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Uratibu wa Misaada ya Kibinadamu (OCHA) ilisema hivi karibuni kuwa, Somalia inaendelea kuandamwa na ukame ambao umeathiri watu zaidi ya milioni 4.3 katika nchi hiyo ya Pembe ya Afrika, kutoka watu milioni 3.2 iliyoripotiwa mwezi mmoja uliopita.