Umoja wa Afrika wakosoa kasi ndogo ya ufungamano barani Afrika
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i8107-umoja_wa_afrika_wakosoa_kasi_ndogo_ya_ufungamano_barani_afrika
Umoja wa Afrika umelalamika kuhusu kasi ndogo ya kuelekea kwenye mafungamano ya bara la Afrika.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
May 30, 2016 03:02 UTC
  • Umoja wa Afrika wakosoa kasi ndogo ya ufungamano barani Afrika

Umoja wa Afrika umelalamika kuhusu kasi ndogo ya kuelekea kwenye mafungamano ya bara la Afrika.

Naibu mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika Erastus Mwencha amesema sababu ya kasi hiyo ndogo, ni baadhi ya nchi za Afrika kuwa na wasiwasi kwamba zinaweza kuingia hasara ikiwa Afrika itakuwa na soko moja.

Akizungumza mjini Nairobi baada ya kumalizika mkutano wa siku tano kuhusu utafiti wa uchumi wa Afrika uliowakutanisha watafiti, wanataalum na watunga sera, Mwencha amesema watafiti wanatakiwa kuonyesha takwimu za vipi nchi za Afrika zitanufaika zikianza kutekeleza soko huru.

Mwencha amesema ni vigumu sana kufanya biashara kati ya nchi za Afrika, na kukumbusha kuwa biashara ya ndani ya nchi za Afrika kwa sasa ni asilimia 12 tu, lakini katika kanda nyingine biashara hiyo ni asilimia 50. Hali hii inatokana na kuwa njia za biashara za nchi za Afrika zilisanifiwa kusafirisha bidhaa kutoka Afrika hadi kwenye mabara mengine.