Askari 7 wa DRC wahukumiwa kifo kwa 'woga' mkabala wa M23
(last modified Mon, 13 Feb 2023 02:34:45 GMT )
Feb 13, 2023 02:34 UTC
  • Askari 7 wa DRC wahukumiwa kifo kwa 'woga' mkabala wa M23

Mahakama moja huko mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo imewahukumu kifo wanajeshi saba wa nchi hiyo, baada ya kupatikana na hatia ya kukimbia medani ya vita na kufanya mauaji.

Inaarifiwa kuwa, askari hao wa serikali ya DRC walivunja viapo vyao na kukimbia medani ya vita katika mji wa Sake, ili wasikabiliane na waasi wa M23. Hukumu ya kifo huko DRC mara nyingi hubadilishwa na kuwa kifungo cha maisha jela. 

Habari zaidi zinaarifu kuwa, wanajeshi hao saba wamepatikana na hatia pia katika shitaka la pili, la kutumia silaha za moto visivyo na kuua raia wawili mjini Sake katika jimbo la Kivu Kaskazini. Mawakili wa askari hao wamesema wataka rufaa kupinga hukumu hiyo.

Novemba mwaka jana, wanajeshi wengine watatu wa Kongo DR walihukumiwa kifo, baada ya kupatikana na hatia ya kukimbia medani ya vita ili wasipambane na waasi wa M23.

Mapigano yameendelea kuripotiwa kati ya jeshi la serikali nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na waasi wa kundi la M23 mashariki mwa nchi hiyo, ambapo kwa sasa mapigano hayo yameshika kasi kwenye eneo la Sake jimboni Kivu Kaskazini.

Wapiganaji wa M23

Mapigano hayo yamesababisha wakazi wengi wa Sake kukimbilia makao makuu ya Kivu kaskazini, Goma, huku wengine wakikimbilia jimbo la Kivu Kusini. 

Mzozo huo umechochea mvutano wa kikanda huku Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ikiituhumu jirani yake Rwanda kwamba inaunga mkono na kufadhili uasi unaoongozwa na Watutsi. 

Tags