Rais wa Iran: Israel inataka kudhoofisha umoja wa umma wa Kiislamu
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i128348-rais_wa_iran_israel_inataka_kudhoofisha_umoja_wa_umma_wa_kiislamu
Rais Masoud Pezeshkian wa Iran amesisitiza kuwa, utawala wa Kizayuni wa Israel unalenga kudhoofisha na kuzusha migawanyiko miongoni mwa mataifa ya Kiislamu.
(last modified 2026-02-09T08:50:53+00:00 )
Jul 15, 2025 04:58 UTC
  • Rais wa Iran: Israel inataka kudhoofisha umoja wa umma wa Kiislamu

Rais Masoud Pezeshkian wa Iran amesisitiza kuwa, utawala wa Kizayuni wa Israel unalenga kudhoofisha na kuzusha migawanyiko miongoni mwa mataifa ya Kiislamu.

Katika kikao na Waziri wa Mambo ya Ndani wa Pakistan, Mohsin Naqvi jana Jumatatu hapa Tehran, Rais Pezeshkian alisisitiza kwamba wanasiasa na wafanya maamuzi katika ulimwengu wa Kiislamu wanapaswa kutambua stratejia hiyo mbovu ya utawala wa Kizayuni na kukabiliana nayo kwa kuimarisha umoja na mshikamano kati ya mataifa ya Kiislamu.

Huku akisisitiza kuwa, utawala wa Kizayuni unalenga kuidhoofisha na kuisambaratisha jamii ya Waislamu, Rais wa Iran amesisitiza kuwa, viongozi na watunga sera katika ulimwengu wa Kiislamu wanapaswa kuwa macho dhidi ya stratejia hiyo mbovu na kufanya kazi ya kuizima kwa kuzidisha mshikamano na mshikamano baina ya mataifa ya Kiislamu.

Akiashiria hali mbaya ya ulimwengu wa Kiislamu, ameutaja umoja na mashirikiano baina ya nchi za Kiislamu kuwa ni jambo la dharura na lisilopingika na kuongeza kuwa, iwapo serikali na mataifa ya Kiislamu yataelewa kikamilifu umuhimu wa umoja wa Kiislamu, yanaweza kusimama kidete kukabiliana na utawala wa Kizayuni unaoendelea kuzusha mifarakano na kufanya ukatili katika jamii za Kiislamu.

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Ndani wa Pakistan amewasilisha salamu za Waziri Mkuu wa nchi yake, Shehbaz Sharif kwa Rais Pezeshkian na kulipongeza taifa la Iran kwa ushindi wake dhidi ya uvamizi wa utawala wa Kizayuni.

Vile vile amekumbusha kuwa Pakistan ilikuwa miongoni mwa nchi za kwanza duniani kulaani uchokozi wa utawala wa Kizayuni dhidi ya Iran, na kuunga mkono haki halali ya Jamhuri ya Kiislamu ya kujilinda.