Kiongozi wa Mapinduzi: Israel ni utawala unaodharaulika na uliotengwa pakubwa duniani
Ayatullah Sayyid Ali Khamenei Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran ameitaja Israel kama utawala unaochukiwa zaidi duniani.
"Hii leo utawala muovu wa Kizayuni ndio utawala unaodharauliwa na uliotengwa pakubwa duniani," lilisomeka chapisho lililowekwa katika mtandao wa kijamii wa X wa KHAMENEI.IR, akaunti rasmi ya Ayatullah Khamenei na majukwaa mengine ya mitandao ya kijamii.
Chapisho hilo ambalo lilirushwa jana mtandaoni kwa lugha za Kifarsi, Kiingereza na Kiebrania liliambatanishwa na picha ya Benjamin Netanyahu Waziri Mkuu wa utawala wa Kizayuni alipokuwa akihutubia Mkutano wa 80 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mjini New York mbele ya safu ya viti vitupu.
Israel kila uchao inazidi kutengwa kimataifa kutokana na vita na mauaji ya kimbari inayofanya dhidi ya wakazi wa Ukanda wa Gaza, ambapo hadi sasa zaidi ya Wapalestina 65,000 wameuawa shahidi au kupoteza maisha kutokana na njaa iliyosababishwa kwa makusudi na Israel tangu ilipoanzisha vita Oktoba 7, 2023.
Maafisa wa Gaza wameeleza kuwa idadi halisi ya vifo katika eneo hilo lililowekewa mzingiro ni kubwa zaidi, kwani wahanga wengi wa mauaji ya kimbari yanayofanywa na Israel wamesalia chini ya vifusi.