Jan 01, 2017 08:10 UTC
  • Iran yalaani hujuma ya kigaidi Uturuki, idadi ya waliouawa yaongezeka

Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imelaani hujuma ya kigaidi iliyofanyika usiku wa kuamkia leo katika mji wa Istanbul nchini Uturuki.

Bahram Qassemi, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran ametuma salamu za rambirambi kwa serikali, wahanga wa hujuma hiyo na taifa la Uturuki kwa ujumla kufuatia shambulizi hilo lilioua makumi ya watu.

Amesema misimamo ya kindumakuwili imesababisha jinamizi la ugaidi kutamalaki katika kila kona ya dunia, bila ya kujali mipaka ya kijiografia, kisiasa, kijamii na kidini.

Ambulensi na timu za waokoaji mjini Instabul

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran ameongeza kuwa, umoja miongoni mwa nchi zote, kushirikiana serikali za nchi hizo na wananchi kuwa macho ni miongoni mwa mambo yanayoweza kusaidia kutokomeza donda ndugu la ugaidi duniani.

Haya yanajrii huku idadi ya watu waliouwa katika hujuma ya Istanbul ikiongezeka na kufikia watu 39. Vasip Sahin, Gavana wa Istanbul amewaambia waandishi wa habari kuwa, mtu aliyekuwa amevalia nguo za Baba Krismasi (Santa Clause) alimuua afisa wa polisi kabla ya kuingia katika klabu hiyo ambapo mamia ya watu walikuwa wamekusanyika kwa ajili ya kuukaribisha mwaka mpya wa Miladia 2017 na kisha akaanza kuwafyatulia risasi ovyo ambapo ameua watu 39 na kuwajeruhi wengi zaidi ya 70.

Sehemu ya athari za shambulio la kigaidi Baghdad

Kadhalika msemaji wa Wizara ya Mambo ya NJje ya Iran amelaani shambulizi la kigaidi la hapo jana katika barabara yenye shughuli nyingi katika mji mkuu wa Iraq, Baghdad, ambapo watu 28 waliuawa na wengine 53 kujeruhiwa. Magaidi wa kundi la kigaidi na kitakfiri la Daesh wamekiri kuhusika na hujuma ya bomu ya hapo jana mjini Baghdad.

Tags