Takhte-Ravanchi: Iran haitoruhusu kuangaliwa upya JCPOA
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran anayehusika na masuala ya Ulaya na Marekani amesema kuwa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran haitatoa mwanya wa kuchunguzwa upya Mpango Kamili wa Pamoja wa Utekelezaji (JCPOA).
Majid Takhte-Ravanchi amesema leo kuwa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kivyovyote vile haitaruhusu kufanyika jambo hilo na kwamba suala hili si tu la Tehran, bali ni kadhia inayozihusu nchi zinazounda kundi la 5+1. Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran anayehusika na masuala ya Ulaya na Marekani ameyasema hayo ikiwa ni radiamali kwa matamshi ya Rex Tillerson aliyependekezwa kushika nafasi ya Waziri wa Mshauri ya Kigeni wa Marekani aliyetaka kuangaliwa upya makubaliano ya JCPOA. Takhte-Ravanchi ameashiria kikao cha hivi karibuni cha kamisheni ya pamoja ya JCPOA huko Vienna Austria na kuchukuliwa dhamana ya kimaandishi kutoka kwa viongozi wa Marekani kuhusu hatua ya nchi hiyo ya kurefusha vikwazo dhidi ya Iran kuwa haitaathiri makubaliano hayo na kubainisha kuwa, katika kikao hicho kumesisitizwa kuwa makubaliano ya JCPOA yanapasa kutekelezwa kikamilifu.
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran anayehusika na masuala ya Ulaya na Marekani amesisitiza kuwa katika kikao hicho cha Vienna, wanachama wote walikuwa na mtazamo mmoja na Iran. Amesema kivyovyote vile haipasi kutolewa fursa ya kuyafanya makubaliano ya JCPOA yakumbwe na matatizo na kutumiwa vibaya. Tangu kuanza kutekelezwa makubaliano ya JCPOA mwezi Januari mwaka jana, Marekani imekiuka ahadi zake ikiwa moja ya pande zilizosaini makubaliano hayo.