Maadhimisho ya Siku ya Afrika yafanyika katika Chuo Kikuu cha Tehran
Maadhimisho ya Siku ya Afrika yaliyohudhuriwa na mabalozi wa nchi za Afrika waliopo hapa mjini Tehran pamoja na wanachuo na wapenzi wa masuala ya Afrika, yalifanyika jana Alkhamisi katika Chuio Kikuu cha Tehran.
Kwa mujibu wa shirika la habari la wanafunzi wa vyuo vikuu ISNA, katika maadhimisho hayo kumefanyika pia maonyesho ya sanaa za mikono kutoka nchi tofauti za Afrika.
Wanachuo wa nchi mbalimbali za Afrika wanaosoma kwenye vyuo vikuu hapa nchini Iran ndio walioandaa na kuendesha maadhimisho hayo.
Siku ya Jumatano kulifanyika pia maadhimsiho ya Siku ya Afrika yaliyohudhuriwa na Dk Mohammad Javad Zarif, Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran. Maadhimisho hayo yalifanyika katika ofisi ya utafiti wa kisiasa ya wizara hiyo.
Siku ya Afrika inaadhimishwa tarehe 25 Mei kila mwaka. Tarehe 25 Mei 1963 ndipo ulipoasisiwa Umoja wa Nchi Huru za Afrika OAU.
Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ina uhusiano mzuri na wa kirafiki na nchi nyingi za Afrika.