Zarif: Sidhani vita baina ya Iran na Marekani vinakaribia, lakini...
-
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Mohammad Javad Zarif
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Mohammad Javad Zarif amesema hadhani vita baina ya Iran na Marekani vinakaribia lakini ametahadharisha kuwa, kuna 'ajali zinazoweza kutokea' na kubadilika kuwa makabiliano ya kijeshi.
Zarif ameyasema hayo katika mahojiano na gazeti la Independent linalochapishwa mjini London ambapo amefafanua kuwa, makusudio yake wakati anaposema 'ajali zinazoweza kutokea' baina ya Marekani na Iran ni hali ya wasi wasi iliyopo katika Lango Bahari la Hormoz kuhusu kupita meli katika eneo hilo muhimu kistratijia.
Zarif ameashiria tukio la Iran kuwakamata wanajeshi wa Marekani ambao boti zao ziliingia katika mji ya Iran kinyume cha sheria katika Ghuba ya Uajemi mwaka 2016 na kusema matukio kama hayo yanaweza kubadilika na kuwa makabiliano.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran aidha amesema: "kuhusu mabadilishano ya wafungwa Wairani na Wamarekani, Iran iko tayari kubadilishana Wamarekani waliokamatwa Iran na Wairani ambao, kwa kosa la kukiuka vikwazo, wamekamatwa Marekani na maeneo mengine.
Akijibu swali kuhusu sababu yake ya kufanya mahojiano na Televisheni ya Fox News ya Marekani, ambayo ni televisheni aipendayo Rais Donald Trump wa Marekani Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amesema: "Wakati mwingine ni muhimu kufanya mazungumzo na upande wa pili, na katika mahojiano na Fox News nilikuwa nazungumza an wafuasi wa Rais wa Marekani."