Iran yavurumisha makombora ya cruise katika mazoezi ya kijeshi baharini
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i65772-iran_yavurumisha_makombora_ya_cruise_katika_mazoezi_ya_kijeshi_baharini
Jeshi la Majini la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran limevurumisha makombora kadhaa ya cruise katika siku ya pili ya mazoezi makubwa ya kijeshi kusini mwa nchi.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Jan 15, 2021 01:07 UTC
  • Iran yavurumisha makombora ya cruise katika mazoezi ya kijeshi baharini

Jeshi la Majini la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran limevurumisha makombora kadhaa ya cruise katika siku ya pili ya mazoezi makubwa ya kijeshi kusini mwa nchi.

Kwa mujibu wa taarifa, makombora hayo yamelenga eneo lilolokusudiwa kaskazini mwa Bahari ya Hindi. Mazoezi hayo ambayo yamepewa jina la Eqtedar-e-Daryayi 99, yalifanyika kwa muda wa siku mbili na yalimalizika jana katika Bahari ya Oman.

Naibu Kamanda wa Uratibu katika Jeshi la Majini la Iran Admeli Hamzeh-Ali Kaviani ambaye ni msemaji wa mazoezi hayo amesema Iran imepata uwezo mkubwa katika uga wa makombora ya cruise na kwamba jeshi lina aina nyingi za makombora hayo. Amesema uwezo mkubwa wa makombora ya cruise umeyafanya yawe ni silaha muhimu katika vita vya majini.

Aidha amesema taarifa za baadhi ya silaha zilizotumika katika mazoezi hayo ni za siri na hazijatangazwa hadharini lakini amewaonya maadui wa Iran kuwa, wakithubutu kukiuka mipaka ya majini ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, basi watakumbana na makombora ya cruise kutokea pwani na baharini.

Meli ya kivita ya Jeshi la Majini la Iran inayojulikana kama Makran ambayo ina uwezo wa kubeba helikopta

Hali kadhalika katika mazoezi hayo Jeshi la Majini la Iran lilitumia nyambizi ya Fateh ambayo imeundwa kikamilifu nchini Iran. Nyambizi hiyo ilivurumisha kwa mafanikio makombora yanayojulikana kama torpedo kutoka kina cha bahari. Katika siku ya kwanza ya mazoezi hayo Jumatano, Iran ilizindua meli yake kubwa kabisa ya kivita inayojulikana kama Makran ambayo ina uwezo wa kusheheni helikopta na ndege zisizo na rubani. Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inasisitiza kuwa uwezo wake wa kijeshi una ujumbe wa urafiki na usalama kwa nchi za eneo na kwa maadui ni onyo kuwa wasithubutu kuanzisha uchokozi dhidi ya Iran.