Apr 21, 2024 11:51 UTC
  • Wapiganaji wa Kiislamu Iraq walenga kambi ya jeshi la Israel kuunga mkono Wapalestina

Harakati ya Muqawama wa Kiislamu ya Iraq imetangaza kulenga ngome "muhimu" ya utawala haramu wa Israel katika Milima ya Golan ya Syria inayokaliwa kwa mabavu na utawala huo ghasibu.

Harakati hiyo inayoyaleta pamoja makundi yote ya Kiislamu yanayopambana na ugaidi Iraq imetoa taarifa ikisema imelenga ngome hiyo ya Israel kwa kutumia ndege za kivita zisizo na rubani.

Harakati hiyo imesemaa operesheni hiyo  ni "katika kuendeleza vita dhidi ya utawala wa Kizayuni wa Israel na kuunga mkono watu wetu huko Gaza wanaokabiliwa na mauaji ya kimbari yanayotekelezwa na Israel.

Hivi karibuni pia Harakati ya Kiislamu ya Iraq ilitangaza kuwa imeshambulia maeneo muhimu katika mji wa Eilat, ulioko kusini mwa Palestina inayokaliwa kwa mabavu. Aidha wapiganaji hao wa Muqawama wa Kiislamu wa Iraq wamelenga Kambi ya Anga ya 'Ovda' ya Wazayuni katika maeneo yanayokaliwa kwa mabavu kwa kutumia ndege zisizo na rubani (drone).

Wapiganaji wa Harakati ya Muqawama wa Kiislamu ya Iraq 

Muungano wa Makundi ya Muqawama nchini Iraq umekuwa ukifanya mashambulizi mengi kama hayo dhidi ya maeneo ya utawala wa Israel, tangu utawala huo unaoikalia kwa mabavu Palestina, uanzishe vita na mauaji ya halaiki huko ukanda wa  Gaza mwezi Oktoba 7.

Sambamba na kuendelea mashambulizi ya jeshi la utawala wa Kizayuni wa Israel dhidi ya Gaza na kukataa kukubali usitishaji vita, vikosi vya muqawama (mapambano ya Kiislamu) ndani na nje ya Palestina pia vimeongeza nguvu na wigo wa mashambulizi ya kujihami dhidi ya utawala huo katili. Vikosi hivyo vya muqawama ni pamoja na vile vya Iraq, Lebanon na Yemen.