Shambulio la anga la Israel laua na kujeruhi Wapalestina wengine 34 Nuseirat na Khan Yunis
Aug 31, 2024 07:40 UTC
Wapalestina wasiopungua 34 wameuawa na kujeruhiwa katika mashambulizi ya anga yaliyofanywa na jeshi la utawala haramu wa Kizayuni wa Israel katika kambi ya Nuseirat na mji wa Khan Yunis katikati na kusini mwa Ukanda wa Ghaza.
Kwa mujibu wa Kituo cha Habari cha Palestina, jeshi la utawala wa Kizayuni limeendeleza jinai zake katika Ukanda wa Ghaza kwa kushambulia kwa mabomu majengo mawili ya makazi katika kambi ya Nuseirat na mji wa Khan Yunis katikati na kusini mwa ukanda huo.
Kufuatia mashambulizi hayo, Wapalestina tisa wameuawa shahidi katika kambi ya Nusairat na wengine watano katika mji wa Khan Yunis. Zaidi ya watu 20 pia wamejeruhiwa katika mashambulizi hayo.

Katika upande mwingine, Shirika la habari la Palestina la Sama limelinukuu gazeti la Kizayuni la Yedioth Ahronoth na kuripoti kuwa, mwanamapambano mmoja wa Kipalestina usiku wa kuamkia leo alijipenyeza katika kitongoji cha Karmei Tzur baada ya kumzidi nguvu mlinzi wa kitongoji hicho na kuwajeruhi Wazayuni wawili.
Kwa mujibu wa Yedioth Ahronoth, operesheni ya ufyatulianaji risasi katika kitongoji cha Karmei Tzur ilitokea baada ya mripuko wa bomu lililotegwa kwenye gari uliotokea kwenye makutano ya Gush Etzion, ambacho ni kitongoji kilichoko kaskazini mwa Al-Khalil, kusini mwa Ukingo wa Magharibi.
Wakati huohuo, vyombo vya habari vya Israel vimeripoti kuwa, Wazayuni wasiopungua sita wamejeruhiwa katika operesheni ya utumiaji silaha baridi iliyotekelezwa kwenye kivuko cha Misri cha Taba.../