Hamas: Vitisho vya Marekani vinatatiza zaidi hali ya mambo
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i124030-hamas_vitisho_vya_marekani_vinatatiza_zaidi_hali_ya_mambo
Msemaji wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (Hamas) amesisitiza kuwa: Vitisho vya Marekani vinapelekea tu hali ya mambo kuwa ngumu zaidi.
(last modified 2025-03-17T08:13:02+00:00 )
Mar 17, 2025 08:13 UTC
  • Hamas: Vitisho vya Marekani vinatatiza zaidi hali ya mambo

Msemaji wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (Hamas) amesisitiza kuwa: Vitisho vya Marekani vinapelekea tu hali ya mambo kuwa ngumu zaidi.

Hazim Qassim ameeleza haya baada ya Steve Witkoff Mjumbe Maalumu wa Marekani katika Mashariki ya Kati, kusema kuwa jibu la Hamas kwa mapendekezo yetu halikubaliki na kwamba eti anaishauri Hamas kuchukua hatua kwa busara zaidi.

Hazim Qassim pia amesisitiza katika mazungumzo na gazeti la al Arabi al Jadid akijibu vitisho vya Steve witkoff kwamba: Kuzungumza kuhusu mapendekezo mapya si kwa maslahi ya utekelezaji wa makubaliano na vitisho vinaifanya hali ya mambo kuwa ngumu zaidi na haviandai mazingira mazuri ya kutekelezwa makubaliano na kurejesha amani katika eneo suala ambalo linafuatiliwa na pande zote.

Qassim amekumbusha kuwa Hamas inasisitiza kuwa kuna makubaliano ambayo pande zote zilitia saini, na makubaliano haya yalifikiwa kupitia Marekani na wajumbe wake, akiwemo Witkoff. 

Hazim Qassim ameongeza kuwa makubaliano haya yanajumuisha marhala tatu na jambo la kufanyika wazi ni kuzingatia utekelezaji wa makubaliano hayo na kuhamia katika marhala ya pili. Msimamo wa serikali ya Kizayuni ya mrengo wa kulia ambayo inaogopa kuingia katika marhala ya pili ya makubaliano kati yake na Hamas, umeibua vizuizi mkabala wa mazungumzo hayo.