Operesheni za kuukomboa mji wa Mosul kutoka kwa Daesh zaanza
Mashambulizi ya kila upande ya jeshi la Iraq kwa kushirikiana na harakati za wanchi kwa ajili ya kuukomboa mji wa Mosul kutoka mikononi mwa wanachama wa genge la kigaidi na ukufurishaji la Daesh (ISIS) zimeanza rasmi.
Waziri Mkuu wa Iraq, Haider al-Abadi ametoa idhini ya kuanza rasmi operesheni hizo zinazoongozwa na jeshi la nchi hiyo kwa kushirikiana na wapiganaji wa harakati ya Hashdu sh-Shabi na Peshmerga. Kufuatia idhini hiyo, mapema leo jeshi la Iraq na wapiganaji wa harakati za Hashdu sh-Shabi na Peshmerga wameshambulia vikali maeneo ya wanachama wa genge la Daesh mjini Mosul.
Wakati huo huo, Abdul-Ghani al-Asadi kamanda wa kikosi cha kupambana na ugaidi nchini Iraq, amewataka wakazi wa mji huo kusalia ndani ya nyumba zao. Duru za habari zimeripoti kukimbia wanachama wa genge la Daesh (ISIS) pamoja na familia zao kutoka mji huo kuelekea mji wa Al-Raqqah, Syria.
Eneo la Bashiqa, mashariki mwa Mosul na ambako wapo askari wa Uturuki, halikusalimika na mashambulizi ya jeshi la Iraq katika kuyalenga magari ya misaada kuelekea genge hilo. Mashuhuda wanaripoti kwamba, siku tatu kabla ya kuanza kwa operesheni hizo, wanachama wa Daesh walikata umeme na mawasiliano ya simu kwa lengo la kuwazuia wakazi wa mji huo kuweza kupata habari. Hii ni katika hali ambayo awali serikali ya Iraq ilikuwa imewataka wakazi wa mji huo kuondoka mjini hapo ili kurahisisha operesheni hizo.
Mji wa Mosul ulikaliwa kwa mabavu na wanachama wa kundi hilo la Kiwahabi la Daesh tangu tarehe 10 mwezi Juni mwaka 2014 na kuufanya kuwa makao makuu yake.