Ripoti: Israel huwatia mbaroni mamia ya Waafrika kila mwaka
Gazeti la Kizayuni la Haaretz limeripoti kuwa vyombo vya usalama vya Israel huwakamata na kuwazuilia mamia ya Waafrika kila mwaka, kinyume cha sheria.
Chapisho la jana Jumapili la gazeti hilo limeripoti kuwa, wakimbizi 311 kutoka barani Afrika wamekamatwa na kuwekwa kizuizini pasina kupandishwa kizimbani katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu na Wazayuni, katika kipindi cha miezi 15 iliyopita.
Kwa mujibu wa gazeti hilo, raia 223 wa nchi za Afrika walikamatwa na kuzuiliwa katika jela za kutisha za utawala wa Kizayuni kati ya Januari mwaka jana 2016 na Machi mwaka huu.
Kadhalika raia wengine 88 wa Kiafrika wanaendelea kusota katika magereza ya Israel licha ya kumaliza vifungo vyao.
Reut Michaeli, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Wakimbizi la utawala wa Kizayuni amesema, Israel inawazuilia mamia ya wakimbizi wa Kiafrika bila kuwafikisha mahakamani au bila ya hata kuwapa haki zao za kimsingi kama kuwaainisha mawakili wa kuwatetea.
Vyombo vya usalama vya utawala haramu wa Israel unaozikali kwa mabavu ardhi za Palestina vinatoa visingizio mbalimbali vya kibaguzi, kuhalalisha unyanyasaji wake dhidi ya Waafrika hao.