Maandamano ya wananchi wa Bahrain kuonyesha mshikamano na Sheikh Issa Qassim
Wananchi wa Bahrain kwa mara nyingine tena wameandamana wakionyesha mshikamano wao na Sheikh Issa Qassim, mwanazuoni mtajika wa nchi hiyo.
Sheikh Issa Qassim kiongozi wa kidini mtajika wa madhehebu ya Shia wa nchini Bahrain tarehe 9 mwezi huu wa Julai alipelekwa mjini London Uingereza kwa ajili ya matibabu baada ya kuzingirwa nyumba yake na askari usalama wa utawala wa Aal Khalifa kwa muda wa miaka miwili. Katika maandamano hayo, wakazi wa maeneo mbalimbali ya Bahrain wametoa nara za kupinga siasa za utawala wa Manama na waungaji mkono wake wakionyesha mshikamano wao kwa mwanazuoni mtajika, Sheikh Issa Qassim.
Waandamanaji hao pia wamesisitiza kuwa wafungwa wote wa kisiasa wanapaswa kuachiwa huru na kutilia mkazo ulazima wa kuendelezwa harakati za wananchi ili kuhakikisha kuwa malengo na matwaka yao yanatimia.
Wananchi wa Bahrain wamekuwa wakifanya maandamano ya kupigania haki zao dhidi ya utawala wa Aal Khalifa tangu Februari 14 mwaka 2011. Utawala wa Aal Khalifa umewatia mbaroni viongozi wengi wa upinzani, kuwafutia uraia na kisha kuwahukumu jela vifungo vya muda mrefu.