Makundi ya Kipalestina yakaribisha oparesheni dhidi ya Wazayuni
Makundi ya Muqawama ya Palestina yamekaribisha na kupongeza kufanyika kwa mafanikio oparesheni mpya dhidi ya Wazayuni katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan.
Wanajeshi wawili wa Israel wameuawa leo asubuhi katika oparesheni mpya ya wanamapambano wa Palestina katika ardhi zinazokaliwa kwa mabavu. Shirika la habari la Tasnim limenukuu tovuti ya Palestina al Yaum na kuripoti kuwa kufautia oparesheni hiyo makundi ya wanamapambano wa Palestina yamesisitiza kuwa oparesheni hiyo mpya inathibitisha kwamba, mwelekeo wa wananchi wa Palestina ni kuendeleza mapambano yao na kupigania uhuru dhidi ya maghasibu na walowezi wa Kizayuni.
Harakati ya Taifa ya Ukombozi wa Palestina pia imeeleza kuwa upinzani mkubwa unapaswa kufanyika dhidi ya utawala wa Kizayuni na kwamba kunapasa kufanyika juhudi za pamoja ili kukabiliana na utawala huo.
Katika upande mwingine Daud Shihab afisa wa Ofisi ya Habari ya Harakati ya Jihadul Islami ya Palestina amepongeza oparesheni hizo mpya za karibuni za wanamapambano wa Palestina.