Maandamano ya kupinga serikali yaendelea Bahrain, wanajeshi washambulia kinyama wafungwa
Maandamano ya wananchi wa Bahrain ya kupinga utawala wa kiukoo na kupigania kuwa na utawala wa wananchi yanaendelea huku utawala wa kidikteta wa ukoo wa Aal Khalifa nao ukiendelea kukandamiza raia.
Habari zinasema kuwa, wanajeshi wa ukoo wa Aal Khalifa nchini Bahrain leo Jumamosi wamewavamia, kuwapiga na kuwanyanyasa kinyama wafungwa wa jela ya Jau mjini Manama.
Wanaharakati wa masuala ya sheria na mitandao ya kijamii wa Bahrain wamesema kuwa wamesikitishwa sana na uvamizi huo dhidi ya wafungwa wa kisiasa ambao wanashikiliwa katika mazingira magumu mno katika jela ya Jau.

Jumuiya ya Haki za Binadamu ya Bahrain imesema katika ripoti yake ya leo kwamba, mwezi Mei 2018, iliorodhesha kesi 1,272 za uvunjaji wa haki za binadamu unaofanywa na maafisa wa utawala wa kifalme wa ukoo wa Aal Khalifa huko Bahrain.
Utawala huo wa kidikteta umeshawatia nguvuni zaidi ya raia 11 elfu wa Bahrain kwa tuhuma zisizo na msingi na kuwapokonya uraia wa nchi hiyo.
Wimbi la harakati za mapinduzi na za kupigania utawala wa katiba uliochaguliwa na wananchi lilianza mwezi Februari 2011 nchini Bahrain. Hata hivyo Saudi Arabia ilituma jeshi lake katika kisiwa hicho cha Bahrain na hadi leo hii wanajeshi hao vamizi wanaendelea kukandamiza raia wanaoandamana kwa njia za amani.
