Gazeti la Saudia laitaka Marekani iishambulie Iran, lasema vikwazo havina athari
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i53539-gazeti_la_saudia_laitaka_marekani_iishambulie_iran_lasema_vikwazo_havina_athari
Gazeti la Saudi Arabia lenye mfungamano na utawala wa Aal-Saud limeitaka Marekani ianzishe mashambulizi ya kijeshi dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, likidai kuwa Tehran na Harakati ya Wananchi ya Ansarullah ya Yemen wamehusika na hujuma dhidi ya taasisi za mafuta za shirika la ARAMCO la Saudia.
(last modified 2026-03-17T04:36:21+00:00 )
May 17, 2019 02:49 UTC
  • Gazeti la Saudia laitaka Marekani iishambulie Iran, lasema vikwazo havina athari

Gazeti la Saudi Arabia lenye mfungamano na utawala wa Aal-Saud limeitaka Marekani ianzishe mashambulizi ya kijeshi dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, likidai kuwa Tehran na Harakati ya Wananchi ya Ansarullah ya Yemen wamehusika na hujuma dhidi ya taasisi za mafuta za shirika la ARAMCO la Saudia.

Gazeti la Arab News lilitoa mwito huo jana Alkhamisi na kueleza kuwa, "Ni wazi kwamba vikwazo vya Marekani (dhidi ya Iran) havijawa na taathira zozote, lazima washambuliwe kwa nguvu zote."

Gazeti hilo la Arab News linamilikiwa na Taasisi ya Utafiti na Mauzo ya Saudi Arabia ambayo imekuwa ikiongozwa na watoto wa Mfalme Salman wa Saudia tangu kuasisiwa kwake hadi mwaka 2014.

Itakumbukwa kuwa, Jumanne iliyopita jeshi la Yemen kwa kushirikiana na harakati ya wananchi ya Ansarullah, lilishambulia taasisi muhimu za mafuta za Shirika la Mafuta la Saudia ARAMCO mjini Riyadh na mji wa Yanbu, magharibi mwa nchi. Jeshi la Yemen na harakati hizo zimetangaza kwamba operesheni hizo za kijeshi zimetekelezwa ikiwa ni katika kujibu mwendelezo wa jinai za muungano vamizi wa Saudia dhidi ya nchi yao.

Huku hayo yakiarifiwa, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Pakistan, Mohammad Faisal amekosoa vikali hatua ya Marekani ya kutuma manowari yake kubwa ya kubeba ndege za kivita pamoja na meli za kijeshi katika Ghuba ya Uajemi, akisisitiza kuwa hatua hiyo haijakuwa na matokeo mengine isipokuwa kushadidisha hali ya taharuki katika eneo la Asia Magharibi.

Manowari ya USS Abraham Lincoln katika Ghuba ya Uajemi

Wakati huohuo, Majid Takht-e Ravanchi, Balozi wa Kudumu wa Iran katika Umoja wa Mataifa ameeleza bayana kwamba, Jamhuri ya Kiislamu haioni umuhimu wowote wa kuongezeka hali ya wasiwasi katika eneo, lakini amesisitiza kuwa Tehran ina haki ya kujilinda na kujihami.

Mwanadiplomasia huyo amesema hayo katika mahojiano na idhaa ya Marekani ya National Public Radio (NPR) yaliyorushwa hewani jana na kubainisha kuwa, "Marekani na waitifaki wake katika eneo wanaeneza tuhuma bandia dhidi ya Iran kwa ajili ya kutaka kufanikisha malengo yao. Lakini Iran ina haki ya kuwa macho na kujilinda kutokana na chokochoko zozote."