Jul 02, 2020 12:10 UTC
  • Ripoti: Wanajeshi wa Marekani wanapora mafuta ya Syria

Wanajeshi wa Marekani wamepora shehena ya matrela 30 ya mafuta ya petroli kutoka visima vya mafuta vya Syria na kuyapeleka Iraq.

Kwa mujibu wa shirika rasmi la habari la Syria, SANA, wanajeshi wa Marekani  wamepora mafuta ya Syria kutoka katika visima vya eneo la Al-Jazira kaskazini mashariki mwa nchi hiyo na kutumia matrela yao ya kijeshi kupelekea mafuta hayo nchini Iraq. Visima vya mafuta vya eneo la Al Jazira viko katika eneo ambalo linakaliwa kwa mabavu na wanajeshi wa Marekani nchini Syria.

Kati kati ya mwezi wa Juni pia wanajeshi wa Marekani walionekana wakipora matrela 50 ya mafuta ya Syria na kuyaingiza Iraq kwa njia ya magendo kupitia eneo la Al Walid.

Taarifa zaidi kutoka Syria zinasema Marekani inajenga kituo kipya cha kijeshi katika eneo la Al Jazira ili kuimarisha uwepo wa majeshi yake katika nchi hiyo ya Kiarabu. Imedokezwa kuwa kituo hicho ambacho kitakuwa mashariki mwa Mto Furati katika viunga vya mji wa Al-Hasakah kitakuwa na uwanja wa ndege za kijeshi.

Wanajeshi vamizi wa Marekani wakifanya magendo ya mafuta nchini Syria

Tokea mwaka 2019, Marekani iliingiza wanajeshi wake katika maeneo ya visima vya mafuta vilivyo katika mikoa ya Al Hasakah na  Deir ez-Zor ambayo inadhibitiwa na Wakurdi kaskazini mashariki mwa Syria.

Kamandi ya Wanajeshi wa Marekani katika eneo la Asia Magharibi iliwahi kutangaza kuwa, wanajeshi wa Marekani  watabakia nchini Syria kwa ajili ya kupora utajiri wa mafuta ya nchi hiyo.

Serikali ya Syria inasisitiza kuwa, uwepo wa wanajeshi wa Marekani na waitifaki wake nchini humo ni sawa na kuikalia kwa mabavu nchi hiyo.

 

Tags