Hizbullah ya Lebanon yatungua ndege ya kijasusi ya Israel
Harakati ya Hizbullah ya Lebanon imefanikiwa kutungua ndege isiyo na rubani ya jeshi la utawala wa Kizayuni wa Israel
Katika taarifa, Hizbullah ya Lebanon imesema drone hiyo ya kijasusi ya utawala pandikizi wa Israel imetunguliwa baada ya kuingia kinyume cha sheria katika anga ya nchi hiyo ya Kiarabu, katika mji wa mpakani wa Aita al Shaab.
Harakati hiyo ya muqawama imetangaza kuwa ndege hiyo ya kijasusi na isiyo na rubani ya utawala wa Kizayuni ipo mikononi mwake.
Kama ilivyotazamiwa, Jeshi la utawala haramu wa Israel linadai kuwa ndege yake hiyo isiyo na rubani imedondoka kutokana na hitilafu za kifundi. Msemaji wa jeshi hilo katili amedai kuwa, Tel Aviv haina wasi wasi juu ya uwezekano wa kuvujishwa taarifa zozote muhimu kutoka kwenye chombo hicho.
Mwezi Juni mwaka huu, aliyekuwa Waziri Mkuu wa Lebanon Hassan Diab alisema mwaka jana pekee utawala ghasibu wa Israel ulihujuma mamlaka ya nchi hiyo ya Kiarabu mara 2,290, na kwamba katika miezi mitano ya kwanza ya mwaka huu, utawala huo pandikizi umehujumu mamlaka ya Lebanon mara 374 ardhini, mara 386 baharini na mara 250 angani.
Vikosi vya muqawama katika eneo la Asia Magharibi mara kwa mara vimekuwa vikitungua 'drone' za utawala pandikizi wa Israel, ambazo hutumiwa na utawala huo wa Kizayuni katika operesheni za mauaji na ujasusi. Mbali na Lebanon, ndege hizo zisizo na rubani za utawala haramu wa Israel zimekuwa zikiruka kinyume cha sheria katika anga za Syria na Palestina.