Al Houthi: Saudi Arabia na Imarati ni vinara wa unafiki
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i63130-al_houthi_saudi_arabia_na_imarati_ni_vinara_wa_unafiki
Katibu Mkuu wa harakati ya wananchi wa Yemen ya Ansarullah amesema kuwa Saudi Arabia na Imarati ni vinara wa kambi ya unafiki.
(last modified 2025-11-07T02:31:33+00:00 )
Aug 31, 2020 03:13 UTC
  • Al Houthi: Saudi Arabia na Imarati ni vinara wa unafiki

Katibu Mkuu wa harakati ya wananchi wa Yemen ya Ansarullah amesema kuwa Saudi Arabia na Imarati ni vinara wa kambi ya unafiki.

Sayyid Abdul Malik al Houthi alisema jana katika hotuba yake ya Siku ya Ashura ya kumbukumbu ya mauaji ya mjukuu wa Mtume Muhammad (saw), Imam Hussein (as) kwamba taifa la Yemen kamwe halitajiunga na kambi ya wanafiki ya maadui wake. 

Katibu Mkuu wa Ansarullah amesema kuwa mapambano ya Wayemeni dhidi ya wavamizi wa nchi hiyo yanatokana na msimamo imara wenye misingi katika mafundisho ya kidini na Kiislamu na kuongeza kuwa: Wananchi wa Yemen wataendeleza mapambano ya kulinda nchi yao katika mazingira na hali zote. 

Abdul Malik al Houthi amesema kuwa mapambano ya Wayemeni dhidi ya uvamizi wa Marekani, Saudia, Imarati na Wazayuni ni jihadi tukufu na wajibu wa kidini, kibinadamu na kitaifa. Amesisitiza kuwa wenzo pekee unaoweza kudhamini uhuru na kujitawala mataifa ya Kiislamu ni kufuata nyayo za Imam Hussein na mafundisho ya Mtume Muhammad (saw).

Siku ya Ashura yaani tarehe 10 Mfunguo Nne Muharram inakumbusha tukio chungu la kuuawa shahidi mjukuu wa Mtume Muhammad (saw), Imam Hussein bin Ali bin Abi Twalib (as) katika eneo la Karbala huko Iraq mwaka 61 Hijria. 

Siku hiyo Imam Hussein (as) na masahaba zake waaminifu walisimama kishujaa kupambana na utawala dhalimu wa Yazid bin Muawiya kwa ajili ya kutetea dini ya Uislamu na mafundisho sahihi ya Mtume Muhammad (saw), na wote wakauawa shahidi katika njia ya Mwenyezi Mungu.