Ushirikiano wa genge la kigaidi la ISIS na Marekani wazidi kufichuliwa
Televisheni moja ya Iraq imesambamba nyaraka mpya zinazoonesha kuweko ushirikiano mkubwa baina ya genge la kigaidi na ukufurishaji la Daesh (ISIS) na Shirika la Kijasusi la Marekani, CIA.
Kanali ya televisheni ya al Furat ya Iraq leo Ijumaa imesambaza nyaraka mpya zinazoonesha kuweko ushirikiano mkubwa baina ya mkuu mpya wa magaidi wa ISIS, Abu Ibrahim al Hashimi al Qurashi maarufu kwa jina la Abu Ibrahim al Qurashi, na shirika la kijasusi la Marekani, CIA. Nyaraka hizo zinaonesha kuwa, mwaka 2008, al Qurashi aliwapa Wamarekani taarifa nyingi za kijasusi.
Kwa mujibu wa nyaraka hizo, wanajeshi magaidi wa Marekani walikuwa wanatumia jela ya Buka huko Iraq kutoa mafunzo kwa wanachama wa genge la kigaidi la Daesh.
Televisheni hiyo ya al Furat imeendelea kufichua kwamba, sababu iliyopelekea genge la kigaidi la Daesh (ISIS) kupata nguvu sana nchini Iraq katika miaka ya 2007 na 2008 ni mafunzo waliyokuwa wakiyapata kutoka kwa wanajeshi vamizi wa Marekani.
Mwaka 2019 genge hilo la ukufurishaji lilimteua Abu Ibrahim al Qurashi kuwa kiongozi wake baada ya kuuawa kiongozi wa zamani wa genge hilo, Aboubakar al Baghdadi.
Mkuu wa zamani wa ISIS, Aboubakar al Baghdadi aliuawa mwezi Oktoba 2019 kaskazini magharibi mwa Syria katika operesheni moja ya kijeshi.