Sheikh Isa Qassim aunga mkono wafungwa wa kisiasa Bahrain
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i65793-sheikh_isa_qassim_aunga_mkono_wafungwa_wa_kisiasa_bahrain
Kiongozi wa Harakati ya Kiislamu ya Bahrain ametangaza kuwaunga mkono wafungwa wote wa kisiasa na watetezi wa haki za binadamu huku akisema kuwa wako katika nyoyo za Wabahrain na katu hawatasahauliwa.
(last modified 2026-04-19T09:26:01+00:00 )
Jan 16, 2021 04:03 UTC
  • Sheikh Isa Qassim aunga mkono wafungwa wa kisiasa Bahrain

Kiongozi wa Harakati ya Kiislamu ya Bahrain ametangaza kuwaunga mkono wafungwa wote wa kisiasa na watetezi wa haki za binadamu huku akisema kuwa wako katika nyoyo za Wabahrain na katu hawatasahauliwa.

Sheikh Isa Qassim ametoa taarifa siku ya Ijumaa ambapo ameashiria hatua ya utawala wa kiimla wa Aal Khalifa  kumkamata Sheikh Zuhair Ashour, mtetezi maarufu wa haki za binaadamu ambapo amemtaja kuwa miongoni mwa watetezi wakuu wa haki za kisiasa za Wabaharian.

Sheikh Qassem amesema kuwekwa kizuizini Sheikh Zuhair Ashour na kuendelea kushikiliwa wafungwa wengine wa kisiasa ni sawa na ukiukwaji wa uhuru na haki za watu wote wa Bahrain.

Aidha ameutaka utawala wa Aal Khalifa uwaachilie huru wafungwa wote wa kisiasa nchini Bahrain. Familia ya Sheikh Zuhair Ashour ina wasiwasi kuhusu hatima yake kwani haina taarifa kumuhusu miezi sita baada ya kukamatwa kwake.

Wananchi wenye hasira wa Bahrain wakiwa na bango la kumpinga mtawala wa nchi hiyo Hamad bin Isa bin Salman Aal Khalifa 

Tangu Februari mwaka 2011, wakati ulipoanza mwamko wa Kiislamu Asia Magharibi, Bahrain imekuwa uwanja wa maandamano ya amani ya wananchi wanaopinga utawala wa kifalme wa ukoo wa Aal Khalifa.

Wananchi hao wanataka kuwepo uhuru, uadilifu, ukomeshwe ubaguzi na kuundwe serikali itakayochaguliwa na wananchi wenyewe.

Hata hivyo kwa msaada wa wanajeshi wa Saudi Arabia na askari usalama wa Imarati (UAE) waliotumwa nchini Bahrain kupitia mpango wa ulinzi wa Ngao ya Kisiwa, utawala wa Aal Khalifa unatumia mkono wa chuma kukabiliana na matakwa ya wananchi hao.

Kwa mujibu wa duru za haki za binadamu, Bahrain ina idadi kubwa zaidi ya wafungwa wa kisiasa kulinganisha na idadi ya watu katika nchi hiyo ndogo zaidi katika Ghuba ya Uajemi.