US kusitisha msaada wa kijeshi kwa Saudia dhidi ya Yemen?
Kufuatia malalamiko na makelele ya jamii ya kimataifa, Marekani imesema inaangalia upya iwapo itaendelea kuipa Saudi Arabia msaada wa kijeshi katika hujuma zake za anga dhidi ya Yemen au la.
Ned Price, msemaji wa Ikulu ya White House katika Baraza la Usalama wa Taifa amesema eti Marekani imeghadhabishwa mno na hujuma ya anga dhidi ya umati mkubwa wa watu waliokuwa wamekusanyika kwenye ukumbi jijini Sana'a kwa ajili ya shughuli ya mazishi hapo jana, ambapo mamia miongoni mwao waliuawa na wengine wengi kujeruhiwa.
Price amesema jinai za kivita zinazotekelezwa na Saudia dhidi ya jirani yake Yemen zinakinzana na 'thamani' na sera za Marekani na kusisitiza kuwa Washington iko tayari kutathmini upya msaada wake wa kijeshi kwa Saudia madhali mgogoro wa Yemen utapatiwa ufumbuzi wa kudumu.
Hii ni katika hali ambayo, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran Bahram Qassemi amebainisha masikitiko yake kufuatia jinai hiyo ya kinyama na iliyo dhidi ya binadamu ya Saudia na kuongeza kuwa, Jamhuri ya Kiislamu inafungamana na familia za waliouawa katika kipindi hiki cha majonzi.
Watu zaidi ya 160 waliuawa baada ya ndege za kijeshi za Saudi Arabia kuwashambulia raia waliokuwa katika shughuli ya mazishi jana Alasiri katika mji mkuu wa Yemen Sana'a.