Mgomo wafuta mamia ya safari za ndege barani Ulaya
https://parstoday.ir/sw/news/world-i26022-mgomo_wafuta_mamia_ya_safari_za_ndege_barani_ulaya
Mgomo wa wafanyakazi katika viwanja vya ndege na mashirika ya ndege barani Ulaya umepelekea kufutwa mamia ya safari barani humo, hatua ambayo imesababisha usumbufu mkubwa kwa wasafiri.
(last modified 2026-05-20T03:07:53+00:00 )
Mar 06, 2017 11:10 UTC
  • Mgomo wafuta mamia ya safari za ndege barani Ulaya

Mgomo wa wafanyakazi katika viwanja vya ndege na mashirika ya ndege barani Ulaya umepelekea kufutwa mamia ya safari barani humo, hatua ambayo imesababisha usumbufu mkubwa kwa wasafiri.

Gazeti la Independet limeandika kuwa, Shirika la Ndege la Britishi Airways leo limefuta safari zake 40 kutokana na mgomo wa wafanyakazi wa kitengo cha minara ya kuongozea ndege cha Ufaransa pamoja na mgomo wa wahudumu wa ndege wa shirika hilo.

Inaelezwa kuwa, akthari ya safari hizo za ndege zilizofutwa leo kutokana na mgomo huo ni za kati ya London na miji ya Ufaransa. Mbali na Ufaransa, safari nyingine sita za ndege zimefutwa leo zikiwa ni za kati ya Uwanja wa Ndege wa Heathrow wa mjini London Uingereza na Barcelona Uhispania na vile vile Milan Italia. Aidha safari za kutoka London kuelekea katika miji mikubwa mitatu ya Uswisi yaani Zurich, Basel na Geneva nazo zimefutwa leo kutokana na mgomo huo.

Ndege ya Shirika la British Airways

Shirika la Ndege la Ufaransa Air France nalo leo limelazimika kufuta safari zake nyingi za ndani za kutokea Paris au za kuelekea katika mji mkuu huo.

Mgomo wa wafanyakazi wa kitengo cha minara ya kuongozea ndege nchini Ufaransa unatarajiwa kuendelea hadi tarehe 10 mwezi huu wa Machi. Wafanyakazi hao wamegoma wakilalamikia kiwango kidogo mshahara.

Wafanyakazi hao wa kituo cha minara ya kuongozea ndege nchini Ufaransa wanasema kuwa, wenzao walioko Ujerumani wamekuwa wakilipwa mshahara mkubwa kuliko wao tena huku kazi zao zikiwa ni chache ikilinganishwa na wao.