Mwana wa Muhammad Ali akamatwa tena Marekani kwa kuwa ni Muislamu
Mwana wa aliyekuwa bingwa wa masumbwi duniani marehemu Muhammad Ali, amekamtwa na kusailiwa tena katika uwanja wa ndege wa mji mkuu wa Marekani, Washington, DC kabla ya kuruhusiwa kupanda ndege.
Muhammad Ali Junior alishikiliwa kwa muda Ijumaa wakati akitaka kupanda ndege ya Shirika la JetBlue akiwa safarini kuelekea Fort Lauderdale na kusailiwa kwa muda wa dakika 20 na maafisa usalama wa Marekani. Wakili wake, Chris Mancini amesema Muhammad Ali alilazimika kuzunguma na maafisa wa Wizara ya Usalama wa Ndani Marekani na kuonyesha leseni yake ya kuendesha gari kabla ya kuruhusiwa kupanda ndege.
Tukio hilo limejiri karibu mwezi mmoja baada ya Ali, na mama yake, Khalila Camacho Ali, wote raia wa kuzaliwa Marekani, kushikiliwa kwa masaa mawili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Fort Lauderdale-Hollywood, tarehe 7 Februari wakati walipokuwa wakirejea Marekani kutoka nchini Jamaica. Katika tukio hilo maafisa wa usalama walitaka kujua iwapo Muhammad Ali ni Muislamu na alitoa wapi jina lake hilo.
Tukio hilo la Ijumaa limejiri wakati Ali na mama yake Jumatano walifika mjini Washington kwa ajili ya kuzungumza na kamati maalumu ya Bunge la Kongresi kuhusu usalama wa mipakani na masaibu waliyokumbana nayo Februari ambayo yanaashiria ubaguzi kwa msingi wa dini.
Ali anasema, hatua yake ya kufika bungeni kulalamika imewakasirisha maafisa wa Wizara ya Usalama wa Ndani Marekani. Wakili Manchini amesema, familia ya Ali inaamini kuwa wanadhalilishwa kwa sababu ya sera za rais Donald Trump za kuwafukuza Waislamu Marekani.
Ali na mama yake wamesema hapana shaka kuwa wanasumbuliwa na maafisa wa usalama kwa sababu tu wao ni Waislamu na wana majina yanayoonekana kuwa ya Kiarabu.
Wiki hii mabingwa wa zamani wa ndondi Evander Holyfield, Larry Holmes, Roberto Duran na wengine wameanzisha kampeni ya kutetea uhuru wa kuabudu kama njia ya kumuenzi bingwa wa ndondi duniani marehemu Muhammad Ali. Wamesema wanapinga sera za Trump za kuwabagua Waislamu.