Wafanyakazi wa Norway wasusia bidhaa za utawala wa Israel
Jumuiya kubwa zaidi ya wafanyakazi Norway imetangaza kususia bidhaa za utawala wa Kizayuni wa Israel kulalamikia ukandamizaji unaofanya na utawala huo dhidi ya Wapalestina.
Jumuiya ya Mashirika ya Wafanyakazi Norway (LO) imepiga kura ya 197 kwa 117 kuunga mkono harakati ya kimataifa ya kususia Israel kiuchumi, kiutamaduni na kielimu.
Harakati ya Kimataifa ya Kususia Israel BDS, ambayo hutetea haki za Wapalestina, imepongeza hatua hiyo ya Wafanyakazi wa Norway na kusema ni njia muafaka ya kutetea haki za Wapalestina.
BDS imeitaka serikali ya Norway ishinikizwe kukata uhusiano wa kijeshi na Israel na kusitisha ushirikiano na mashirika yote yaliyo na uhusiano na utawala wa Kizayuni wa Israel. Hata hivyo waziri wa mambo ya nje wa Norway Borge Brende amekosoa hatua hiyo.
Harakati ya Kimatiafa ya Kususia Israel BDS ilianzishwa mwaka 2005 na mashirika zaidi ya 170 ya kutetea haki za Palesitna kwa lengo la kuishawishi jamii ya kimataifa iususie utawala wa Kizayuni wa Israel hadi utakapositisha ukandamizaji wa Wapalestina.