Kuongeza mashambulizi ya silaha Marekani, watu 71 waliuawa Jumanne pekee
Katika matukio 82 ya mashambulizi ya silaha za moto nchini Marekani yaliyojiri siku ya Jumanne pekee katika majimbo tofauti nchini humo kwa akali watu 71 wameuawa na wengine 53 kujeruhiwa.
Mashambulizi ya silaha hizo za moto yameripotiwa katika majimbo tofauti yakiwemo ya Pennsylvania, Ohio, Florida na Texas nchini humo. Kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa na kituo cha kukusanya takwimu za vitendo vya utumiaji mabavu wa silaha nchini Marekani, baadhi ya hujuma hizo za silaha za moto zimewahusisha pia watu wa familia moja. Inaarifiwa kuwa ongezeko la mashambulizi hayo ya silaha nchini Marekani limeshika kasi zaidi tangu alipoingia madarakani Rais Donald Trump.
Kadhalika kituo cha kukusanya takwimu za vitendo vya utumiaji mabavu wa silaha nchini Marekani, kimetangaza kuwa, kwa muda wa saa 48 zilizopita jumla ya matukio 247 ya mashambulizi ya silaha hizo yameripotiwa na kusababisha makumi ya watu kuuawa na wengine 155 kujeruhiwa. Kwa mujibu wa ripoti rasmi, karibu silaha za moto milioni 270 hadi milioni 300 ziko mikononi mwa raia. Hii ikiwa na maana kwamba, karibu kila Mmarekani anamiliki silaha, suala ambalo linatishia usalama wa nchi hiyo inayojinadi kuwa polisi wa dunia. Ukosefu wa matumaini na amani inatajwa kuwa sababu ya asilimia kubwa ya Wamarekani kumiliki silaha hizo hatari ambazo hutumika kukatisha maisha yao wenyewe.