Seneta wa Marekani atahadharisha kuhusu kujtoa nchi hiyo katika JCPOA
Seneta wa chama cha Democrat nchini Marekani ametahadharisha kuhusu taathira hasi za kujitoa nchi hiyo katika makubaliano ya JCPOA yaliyofikiwa kati ya Iran na kundi la 5+1.
Ben Cardin amesema kuwa Marekani itapoteza itibari yake iwapo itajitoa katika makubaliano hayo; na ameitaka serikali ya Rais Donald Trump ibakie kwenye makubaliano hayo ya nyuklia yaliyofikiwa kati ya Iran na kundi la 5+1.
Seneta huyo wa chama cha Democrat amesema, kujitoa Marekani katika JCPOA ni hatua isiyo ya kimantiki na kwamba White House haitakuwa tena na itibari mbele ya jamii ya kimataifa kwa kujitoa Marekani katika makubaliano hayo na kukiuka azimio la Umoja wa Mataifa. Akihutubia katika mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa hivi karibuni mjini New York, Rais Donald Trump wa Marekani aliyataja makubaliano hayo kuwa ni fedheha kwa nchi yake.
Kwa upande wake Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Nyuklia (IAEA) umethibitisha katika ripoti zake nane zilizotolewa tangu kuanza kutekelezwa makubaliano ya JCPOA kwamba, Iran imeheshimu ahadi na kutekeleza majukumu yake katika fremu ya makubaliano hayo. Wakati huo huo Mkuu wa Kamandi Kuu ya Majeshi ya Marekani Jenerali Joseph Dunford amebainisha pia kuwa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imetekeleza majukumu yake kuhusu makubaliano ya JCPOA na ametaka Marekani ibaki katika makubaliano hayo kati ya Iran na kundi la 5+1.