Mshauri wa Obama: Trump anaiaibisha Marekani duniani
Al Sharpton, mshauri wa aliyekuwa rais wa Marekani Barack Obama na mwanaharakati mkubwa wa haki za binaadamu nchini Marekani amesema kuwa, Rais Donald Trump amesababisha makundi ya mrengo wa kulia na yenye misimamo mikali kupata nguvu nchini humo.
Al Sharpton ameyasema hayo katika mahojiano na gazeti la Uingereza la Independent na kusema kuwa, matamshi ya uchochezi na yenye kuibua hisia za chuki ya Rais Trump, yamesababisha kushamiri ubaguzi wa rangi na ubaguzi dhidi ya wanawake. Alfred Charles Sharpton ameongeza kwa kusema kuwa, hivi sasa Trump anajaribu kuwarejesha nyuma watu kuhusiana na masuala ya haki za binaadamu, huduma za afya na uhuru na kwamba wanajitahidi kuzuia hilo.
Aidha mwanaharakati huyo wa haki za binaadamu amesisitiza kwamba, ni jambo la kuaibisha kwamba inatulazimu kuwafafanulia Waingereza na watu wa maeneo mengine duniani, ni kwa nini Rais wa Marekani anaandika mambo ya kijinga kabisa na yenye kuibua tofauti kubwa kwenye Twitter na kuishusha hadhi ya Ikulu ya White House. Hii sio mara ya kwanza kwa maafisa wa ngazi ya juu wa Marekani kukosoa mienendo ya kushangaza ya Rais Donald Trump wa nchi hiyo.