Alkhamisi tarehe 7 Septemba 2023
Leo ni َAlkhamisi tarehe 21 Mfunguo Tano Safar 1445 Hijria sawa na tarehe 7 Septemba 2023.
Katika siku kama ya leo miaka 201 iliyopita, nchi ya Brazil ilipata uhuru kutoka kwa mkoloni Mreno. Ureno ilianza kuikoloni Brazil mwaka 1494, na mbali na kuwatumikisha watu wa jamii ya Wahindi Wekundu wa nchi hiyo, ilichukua mamilioni ya Waafrika kwa ajili ya kuwatumikisha kama watumwa katika shughuli za kilimo. *

Siku kama ya leo miaka 124 iliyopita harakati ya kihistoria ya Wanamasumbwi nchini Uchina ilikandamizwa na kuzimwa. Wanamasumbwi lilikuwa jina walilopewa wanajeshi wa China waliosimama kupambana na ubeberu wa nchi za kigeni hususan za Magharibi ulioambatana na harakati za wamishonari wa Kikristo ndani ya China. Miongoni mwa hatua zilizochukuliwa na wanamasumbwi hao ni kuteka balozi za nchi za Magharibi katika mji wa Beijing na kupambana vikali na shughuli za wahubiri wa Kikristo kutoka Ulaya. Harakati ya Wanamasumbwi wa Kichina ilikandamizwa na majeshi ya Ulaya, Marekani na Japan na serikali ya China ikalazimika kulipa gharama kubwa kwa nchi hizo.

Tarehe 16 Shahrivar miaka 39 iliyopita aliaga dunia Ayatullah Mirza Muhammad Baqir Ashtiyani, mmoja wa maulamaa wakubwa wa Iran. Alizaliwa mwaka 1284 Hijria Shamsiya mjini Tehran. Ayatullah Ashtiyani alielekea katika chuo cha kidini cha Najaf nchini Iraq kwa ajili ya kukamilisha masomo baada ya kuhitimu masomo yake ya awali. Ayatullah Mirza Muhammad Baqir Ashtiyani alirudi Tehran na kuanza kutoa elimu kwa wanafunzi wa masuala ya dini baada ya kupata daraja ya ijtihadi. Msomi huyo mkubwa ameandika vitabu vingi vya thamani kama "Uongozi kwa Mtazamo wa Uislamu" na kile cha "Umiliki katika Uislamu".
Siku kama ya leo miaka 26 iliyopita alifariki dunia dikteta wa zamani wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo au Zaire ya zamani, Jenerali Mobutu Sese Seko. Mobutu alizaliwa mwaka 1930 nchini Congo na mwaka 1950 alijiunga na harakati ya ukombozi ya Patrice Lumumba. Baada ya uhuru wa Congo, Jenerali Mobutu alishika uongozi wa jeshi la nchi hiyo na mwaka 1960 alikuwa waziri mkuu akiwa na umri wa miaka 30. Tarehe 25 Novemba mwaka 1965 Mobutu alipindua serikali na kushika hatamu za nchi hiyo aliyeitawala kidikteta. Tarehe 16 Mei 1997 Mobutu alilazimika kukimbia nchi hiyo na kwenda Morocco ambako alifia na kuacha nyuma faili jesi la ukatili na mauaji.