Boko Haram watoa mkanda wa video wa wasichana waliowateka nyara Chibok
Wanamgambo wa kitakfiri wa kundi la Boko Haram wametoa mkanda mpya wa video unawaonyesha baadhi ya wasichana waliotekwa nyara na kundi hilo katika mji wa Chibok Nigeria mwaka 2014.
Katika mkanda huo mpya wa video uliotolewa leo, anaonekana mwanamgambo mmoja wa Boko Haram akidai kuwa baadhi ya wasichana waliowateka nyara wangali hai na kwamba wengine waliuliwa kwenye mashambulizi ya anga ya vikosi vya Nigeria katika ngome ya kundi hilo.
Mwanamgambo huyo wa kitakfiri wa Boko Haram ameongeza kusema, na hapa ninamnukuu,"wanapaswa kufahamu kuwa watoto wao bado wapo mikononi mwetu na baadhi yao waliuawa kwenye mashambulizi ya anga, mwisho wa kunukuu".
Mwanamgambo huyo wa kundi la Boko Haram ameendelea kudai kuwa kuna wasichana wapatao 40 ambao wameolewa. Mwanamgambo huyo ambaye amefunika uso wake katika mkanda huo wa video pia ametaka kuaachiwa huru makamanda wao mkabala na kuwaachia huru wasichana waliowateka nyara huko Chibok. Itakumbukwa kuwa wanamgambo wa kitakfiri wa kundi la Boko Haram mwezi Aprili mwaka juzi waliwateka nyara wasichana 276 katika shule ya sekondari ya mji wa Chibok kaskazini mashariki mwa Nigeria. Hata hivyo wasichana 57 walifanikiwa kutoroka huku wengine karibu 220 wakiwa hawajakulikani walipo. Juhudi za kimataifa za kuwanusuru mabinti hao kutoka mikononi mwa Boko Haram hadi sasa zimegonga mwamba.