Maharamia wateka meli ya mizigo katika pwani ya Somalia
Maharamia wa katika pwani ya Somalia wameiteka meli nyingine ya mizigo kando ya pwani ya nchi hiyo. Hayo ni kwa mujibu wa ripoti za mashirika ya usalama wa baharini. Tukio hili ni ishara mpya ya kurejea kwa uharamia katika maji ya Pembe ya Afrika, baada ya miaka mingi ya utulivu .
Kulingana na kituo cha Operesheni za Biashara ya Baharini cha Uingereza (UKMTO), Meli hiyo ya mizigo yenye bendera ya Cameroon iitwayo Lutuf, ilivamiwa na watu wanane wenye silaha mwendo wa saa 11:36 asubuhi (UTC) mnamo tarehe 17 Agosti 2026, takriban maili nne za baharini kusini mwa Mareeyo, Somalia,
Shirika hilo limeainisha tukio hilo kama utekaji nyara. Kampuni ya usalama wa baharini ya Vanguard Tech imetaja meli hiyo kuwa ni Lutuf, yenye uzito wa tani 1,401, iliyoundwa mwaka 1995. Hali ya wafanyakazi wake bado haijathibitishwa katika ripoti za hivi punde.
Utambulisho na matakwa ya maharamia hao hayajajulikana, na hakuna kundi lolote lililojitokeza hadharani kukiri kuhusika na tukio hilo.
Ripoti ya awali ilitoka kwa afisa usalama wa kampuni ya meli hiyo, ambaye aliliambia UKMTO kuwa watu wanane wasioidhinishwa wenye silaha walivamia na kuchukua udhibiti wa meli hiyo.
Ripoti za awali kwenye mitandao ya kijamii zimedai kuwa wafanyakazi wako salama, lakini taarifa hii haijathibitishwa na UKMTO au ripoti nyingine za kuaminika za baharini zilizopo hadi sasa.
Uharamia katika Pembe ya Afrika ulikuwa umepungua baada ya kushamiri katika miaka ya 2000 na kufikia kilele chake karibu mwaka 2011; lakini mwaka 2026 umeshuhudia ongezeko la shughuli hizo, huku meli kadhaa zikitekwa na maharamia. Meli tatu za mafuta na mbolea zilitekwa mwezi Aprili na Mei, na meli ya kemikali ilitekwa kando ya pwani ya Yemen mwezi Julai. Meli zote nne bado zinashikiliwa kando ya pwani ya Somalia.