Morocco yaangamiza kundi la kigaidi linalofungamana na ISIS
Wakuu wa Morocco wametangaza kufanikiwa kuangamiza kundi moja la kigaidi nchini humo.
Katika taarifa siku ya Jumatano, serikali ya Morocco ilitangaza kuwa, polisi nchini humo wamefanikiwa kuangamiza kundi moja la kigaidi ambalo linafungamana na kundi la kigaidi la ISIS au Daesh kaskazini mwa nchi hiyo.
Taarifa hiyo imesema kuwa, vikosi vya usalama vimefanikiwa kuwakamata watu kadhaa wenye misimamo mikali ambao ni wafuasi wa ISIS katika miji ya Oujda, Saidia, Fez na Debdou.
Kwa mujibu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Morocco, maafisa wa usalama wamefanya upekuzi katika nyumba kadhaa maeneo hayo ambayo wamepata idadi kubwa ya mada za kemikali ambayo zingeweza kutumika kutengeneza mabomu.
Wizara ya Mambo ya Ndani ya Morocco imesema waliokamatwa walikuwa wamepanga kujiunga na magaidi wa ISIS nchini Libya na baada ya hapo kurejea Morocco kutekeleza hujuma za kigaidi.