Ellen Sirleaf: Yahya Jammeh hayuko tayari kuachia madaraka
Wakuu wa nchi za magharibi mwa Afrika ambao wamefanya safari huko Gambia kwa lengo la kusuluhisha mgogoro wa ndani uliojitokeza, jana walitangaza kuwa jitihada zao za kumshawishi Yahya Jammeh akabidhi madaraka bado hazijazaa matunda.
Rais Ellen Johnson Sirleaf wa Liberia ambaye ndiye mwenyekiti wa kiduru wa Jumuiya ya Kiuchumi ya Nchi za Magharibi mwa Afrika (ECOWAS), jana alieleza kuwa ujumbe wa jumuiya hiyo uliotumwa huko Gambia kupatanisha, hadi sasa haujafanikiwa kumshawishi Rais wa sasa wa nchi hiyo Yahya Jammeh akubali matokeo ya uchaguzi wa rais na kuondoka madarakani. Viongozi wa Ecowas wanafanya kila wawezalo ili kumshawishi Jammeh akubali matokeo ya uchaguzi wa Rais katika hali ambayo chama tawala nchini humo jana kiliitaka Mahakama Kuu itangaze matokeo ya uchaguzi wa Rais wa Gambia uliofanyika hivi karibuni kuwa ni batili.
Yahya Jammeh ambaye amekuwa madarakani huko Gambia kwa muda wa miaka 22 awali alikubali matokeo ya uchaguzi wa Rais uliofanyika Disemba Mosi nchini humo, hata hivyo baadaye alibadili msimamo na kupinga matokeo hayo; hatua ambayo imelalamikiwa na jamii ya kimataifa.