Boko Haram washambulia na kuua askari watatu mashariki mwa Nigeria
Askari watatu wa jeshi la Nigeria wameuawa katika shambulio jipya lililofanywa na kundi la kigaidi na kitakfiri la Boko Haram katika eneo moja kaskazini mashariki mwa nchi hiyo.
Ripoti kutoka jimbo la Kano zimenukuu duru za hospitali hapo jana zikitangaza kuwa wanajeshi watatu waliuawa na wengine kadhaa walijeruhiwa katika shambulio lililofanywa na Boko Haram dhidi ya kituo kimoja cha usalama karibu na mji wa Kamuya kaskazini mashariki mwa Nigeria.
Hata hivyo duru zenye mfungamano na kundi hilo la kigaidi na kitakfiri zimedai kuwa askari watano waliuawa na wengine 11 walijeruhiwa katika shambulio hilo.
Kundi la Boko Haram ambalo ni moja ya tishio kubwa la usalama katika eneo la magharibi mwa Afrika lilianzisha harakati zake za uasi mwaka 2009 na kupanua wigo wa hujuma zake mwaka 2015 katika nchi jirani na Nigeria za Niger, Chad na Cameroon.
Zaidi ya watu 17,000 wameuliwa kutokana na hujuma na mashambulio ya kundi hilo la kigaidi na kitakfiri mbali na wengine zaidi ya milioni mbili na laki sita waliobaki bila ya makazi…/