Maelfu waandamana kumpinga rais wa Senegal
Maelfu ya watu wameandamana mjini Dakar, Senegal kupinga siasa za Rais Macky Sall wa nchi hiyo ya magharibi mwa Afrika.
Kwa mujibu wa IRIB, maelfu ya waandamanaji nchini Senegal jana walishiriki katika maandamano ya kuonesha hasira dhidi ya Rais Macky Sall aliyeingia madarakani mwaka 2012. Waandamanaji walivaa nguo nyeusi katika maandamano yao hayo.
Vile vile waandamanaji hao wametaka kuachiliwa huru meya wa Dakar na wapinzani wa chama cha kisoshalisti waliotiwa mbaroni tangu tarehe 7 Machi mwaka huu.
Fadel Barro mratibu wa asasi za kijamii na mmoja wa waandaaji wa maandamano hayo amelaani hatua ya serikali ya nchi hiyo ya kuwatia mbaroni wapinzani.
Senegal ilipata uhuru wake mwaka 1960 kutoka kwa mkoloni wa Ulaya, Ufaransa na kuanzia wakati huo hadi hivi sasa inatawaliwa na mfumo wa jamhuri ya kidemokrasia.
Pamoja na hayo, sehemu kubwa ya mfumo wa utawala nchini humo imeendelea kuwa ile ile ya enzi za ukoloni wa Ufaransa.