Wanajeshi wa Nigeria washambulia maficho ya magaidi wa Boko Haram
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i28596-wanajeshi_wa_nigeria_washambulia_maficho_ya_magaidi_wa_boko_haram
Ndege za kivita za Nigeria zimefanya mashambulizi katika maficho ya wanamgambo wa Boko Haram kaskazini mashariki mwa nchi hiyo ya magharibi mwa Afrika na kuua magaidi kadhaa.
(last modified 2023-11-27T12:14:11+00:00 )
May 03, 2017 14:39 UTC
  • Wanajeshi wa Nigeria washambulia maficho ya magaidi wa Boko Haram

Ndege za kivita za Nigeria zimefanya mashambulizi katika maficho ya wanamgambo wa Boko Haram kaskazini mashariki mwa nchi hiyo ya magharibi mwa Afrika na kuua magaidi kadhaa.

Mtandao wa habari wa All Africa umeripoti habari hiyo na kuongeza kuwa, mashambulizi hayo yamefanyika katika jimbo la Borno, la kaskazini mashariki mwa Nigeria na kuua pia viongozi kadhaa wa kundi hilo la kigaidi.

Kuna wakati jimbo la Borno lilikuwa ngome kuu ya kundi la wakufurishaji la Boko Haram. Kwa mujibu wa ripoti hiyo, serikali ya Nigeria imetuma wanajeshi wengi maalumu katika maeneo ya operesheni za kijeshi za nchi hiyo ili kukabiliana na mashambulizi ya kuvizia ya wanamgambo wa Boko Haram.

Wasichana waliotekwa nyara na kundi la wakufurishaji wa Boko Haram nchini Nigeria

 

Hadi hivi sasa kundi la Boko Haram limeshaua maelfu ya raia, hasa wanawake na watoto wadogo tangu ilipoanzisha mashambulizi yake nchini Nigeria mwaka 2009. Moja ya matukio maovu kabisa yaliyofanywa na genge hilo ni kuwateka nyara mamia ya wanafunzi wa kike huko Chibok na kuwauza kama bidhaa.

Ijapokuwa katika miezi ya hivi karibuni, Nigeria imepata baadhi ya mafanikio katika vita vyake dhidi ya Boko Haram, lakini serikali ya Rais Muhammadu Buhari ya nchi hiyo inaonekana imeshindwa kutimiza ahadi zake za kulimaliza kundi hilo la kitakfiri.

Mwaka 2015, kundi la kigaidi la Boko Haram lilianza kuzishambulia pia nchi jirani za Chad, Cameroon na Niger na hivyo kuzidi kuhatarisha usalama wa eneo zima la Ziwa Chad.