Wapiganaji watatu wa al-Shabab watiwa mbaroni nchini Somalia
Wanachama watatu wa kundi la kigaidi la al-Shabab wametiwa mbaroni nchini Somalia.
Duru za habari zimewanukuu maafisa wa usalama wa Somalia wakitangaza kuwa, wanachama hao wa kundi la kigaidi la al-Shabab walitiwa mbaroni katika operesheni ya jana ya jeshi katika mkoa wa Bakool ulioko kusini magharibi mwa nchi hiyo ya Pembe ya Afrika.
Mohamed Mo'alim mkuu wa mkoa wa Bakoo amesema kuwa, lengo la operesheni hiyo lilikuwa ni kuusafisha mji huo na uwepo wa wapiganaji wa wanamgambo wa al-Shabab. Amesema kuwa, operesheni hiyo ya kijeshi imekuwa na mafanikio makubwa. Inaelezwa kuwa, wanamgambo wa al-Shabab wametega mabomu ya ardhini katika maeneo mbalimbali ya mji huo na hivyo kuhatarisha usalama wa maisha ya watu.
Hayo yanajiri katika hali ambayo, operesheni ya vikosi vya kusimamia amani vya Umoja wa Afrika AMISOM nchini Somalia navyo vimeendelea na operesheni kali dhidi ya wanamgambo wa al-Shabab.
Jumamosi iliyopita jeshi la Kenya linalofanya shughuli zake chini ya mwavuli wa AMISOM liliwaangamiza magaidi 21 wa kundi la kitakfiri la al Shabab kufuatia mapigano makali huko Somalia.
Msemaji wa Jeshi la Kenya KDF Kanali David Obonyo amesema kuwa, wanajeshi wawili wa Kenya pia waliuawa na wengine watano kujeruhiwa katika mapigano hayo makali yaliyojiri mjini Afmadow kusini mwa Somalia.