Mahakama ya Kilele Kenya yaidhinisha ushindi wa Rais Uhuru Kenyatta
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i36571-mahakama_ya_kilele_kenya_yaidhinisha_ushindi_wa_rais_uhuru_kenyatta
Mahakama ya Kilele nchini Kenya imetupilia mbali kesi mbili zilizokuwa zimewasilishwa kupinga uchaguzi wa rais wa marudio wa Oktoba 26 na hivyo kuidhinisha ushindi wa Uhuru Kenyatta.
(last modified 2026-04-19T09:26:01+00:00 )
Nov 20, 2017 11:11 UTC
  • Mahakama ya Kilele Kenya yaidhinisha ushindi wa Rais Uhuru Kenyatta

Mahakama ya Kilele nchini Kenya imetupilia mbali kesi mbili zilizokuwa zimewasilishwa kupinga uchaguzi wa rais wa marudio wa Oktoba 26 na hivyo kuidhinisha ushindi wa Uhuru Kenyatta.

Majaji wote sita wa Mahakama hiyo wameafikiana kwa kauli moja katika uamuzi huo ambao sasa utaandaa mazingira ya Kenyatta kuapishwa kama rais wa Kenya, kwa muhula wa pili mfululizo, katika kipindi cha siku chache zijazo.

Mahakama ya Juu ya Kenya imekuwa kitovu cha siasa za nchi hiyo tangu ilipobatilisha matokeo ya uchaguzi wa mwanzo wa rais uliofanyika Agosti 8 na kupelekea kufanyika uchaguzi mwingine tarehe 26 Oktoba.

Tume Huru ya Uchaguzi IEBC imefurahia uamuzi huo wa Mahakama ya Kilele na kusema ni dhihirisho la kujitolea kwa tume hiyo kufanikisha uchaguzi huru, wa haki na wa kuaminika.

Imesema kupitia taarifa kwamba inasubiri uamuzi wa kina ambao utaiongoza katika kutathmini uchaguzi huo ulivyokuwa pamoja na mipango yake ya kuimarisha uchaguzi na tume yenyewe.

Majaji wa Mahakama Kuu ya Kenya

Kufuatia uamuzi huo, Maandamano yameshuhudiwa katika maeneo yenye wafuasi wengi wa kiongozi wa upinzani Raila Odinga.

Katika mji wa Kisumu, magharibi mwa nchi hiyo, vijana wamejitokeza kuandamana barabarani.

Video zimeonesha gari moja la kibinafsi likiteketea. Muungano wa NASA umetoa taarifa na kusema haumtambui Kenyatta kama rais halali wa Kenya.

Wafuasi wa Rais Kenyatta wamesherehekea uamuzi wa mahakama kwa nyimbo nje ya Mahakama ya Juu na katika maeneo mengine ambayo ni ngome yake.