Kiongozi wa wanaotaka kujitenga Cameroon atiwa nguvuni nchini Nigeria
Kiongozi wa harakati ya wanaotaka kujitenga nchini Cameroon ametiwa nguvuni katika mji mkuu wa nchi jirani ya Nigeria.
Julius Ayuk Tabe mwenyekiti wa kundi la wanaotaka kujitenga la Governing Council of Ambazonia ametiwa nguvuni akiwa katika hoteli moja mjini Abuja akiwa pamoja na wasaidizi wake 6.
Maafisa wa serikali ya Nigeria wanasema kuwa Tabe na wenzake sita walitiwa nguvuni Ijumaa iliyopita katika Hoteli ya Nera ambako walikuwa na mkutano.
Waasi wa kundi hilo wanataka kuunda nchi huru ya "Ambazonia".
Harakati hiyo inayotaka kujitenga ya Wacameroon wanaozungumza lugha ya kiingereza katika nchi hiyo yenye idadi kubwa ya watu wanaozungumza Kifaransa imeshika kasi zaidi katika miezi ya hivi karibuni kufuatia ukandamizaji wa jeshi dhidi ya wafuasi wa harakati hiyo.
Uhusiano wa Nigeria na Cameroon umevurugika na kuingia katika hali ya mivutano baada ya jeshi la Cameroon mwezi uliopita kuvuka mpaka na kuingia katika ardhi ya nchi hiyo jirani kwa ajili ya kuwasaka waasi bila ya kibali cha viongozi husika wa Nigeria.