Mkutano wa Senegal wahimiza kushirikishwa Waislamu wote katika masuala ya Hija
Mkutano wa kimataifa wa Senegal umehimiza kushirikishwa nchi zote za Kiislamu katika usimamiaji wa amali ya Hija.
Kwa mujibu wa shirika la habari la Fars, shakhsia wa kidini na kielimu duniani waliokutana huko Dakar, Senegali katika mkutano wa kimataifa ulioitishwa chini ya kaulimbiu ya "Upeo wa Kisiasa na Kiuchumi wa Usimamiaji wa Saudia wa Nembo Takatifu za Kiislamu na Falsafa ya Hija" wamekosoa vikali jinsi Saudi Arabia inavyotumia vibaya ibada ya Hija kwa malengo ya kisiasa na kiuchumi.
Kamati ya Kimataifa ya Kuchunguza Uendeshaji wa Saudia wa Haram Mbili Takatifu na washiriki wengine wa mkutano huo wa Senegal wametaka nchi zote za Kiislamu zishirikishwe katika usimamiaji na uendeshaji wa amali ya Hija.
Kamati hiyo ya kimataifa ilianza kazi zake mwanzoni mwa mwaka huu wa 2018 kwa shabaha ya kuzuia kutumiwa kisiasa amali ya Hija na kuishinikiza Saudi Arabia isimamie vizuri maeneo matakatifu ya Kiislamu na kuhifadhi muundo na usalama wa maeneo hayo matukufu.
Itakumbukwa kuwa katika maafa yaliyotokea kwenye msimu wa Hija wa mwaka 2015 katika eneo la Mina, mahujaji elfu saba wakiwemo mahujaji 465 wa Iran walipoteza maisha yao kutokana na usimamiaji mbovu wa viongozi wa Saudia.